Tuesday, June 23, 2015

Serikali yakana kumtorosha Rais wa Sudani






 Serikali ya Afrika Kusini imekana ripoti kwamba mawaziri wake walipanga njama ya kumtorosha rais wa Sudan Omar El Bashir wiki iliopita.
 
Katika tukio hilo nusura rais huyo akamatwe kufuatia agizo la mahakama ya kimataifa kuhusu uhalifu wa kivita dhidi yake kutokana na mashtaka ya mauaji ya kimbari.
 
Mahakama ya Afrika Kusini ilimuagiza Bashir kusalia nchini humo huku ikijadiliana kuhusu iwapo agizo hilo litekelezwe. Lakini kabla ya mahakama hiyo kutoa uamuzi wake bwana Bashir aliondoka nchini Afrika Kusini na kurudi nyumbani.
 
Rais huyo wa Sudan alikuwa nchini Afrika Kusini kwa mkutano wa viongozi wa bara Afrika na kwamba serikali ilikuwa inajua kwamba ilihitajika kumkamata kwa kuwa mwanachama wa ICC.
 
Kwa mujibu wa  gazeti la Sunday Times nchini Afrika Kusini limenukuu duru za serikali kwamba katika mkutano wa mawaziri ilikubalika kwamba Afrika Kusini itamlinda hata iwapo italazimika kukiuka uamuzi wa mahakama na kukiuka katiba.
 
Katika taarifa yake,serikali imekana kwamba kulikuwa na mkutano wa siri na kwamba itaipatia mahakama hiyo maelezo kuhusu vile Bashir alivyoondoka nchini humo.
 
Mahakama kuu imeipatia serikali ya taifa hilo hadi alhamisi kubaini ni vipi aliruhusiwa kuondoka.

No comments:

Post a Comment

Popular Posts