Saturday, January 24, 2015

Madereva wa daladala wamefunga barabara mkoani Mwanza




Maelfu ya wakazi wa jiji la Mwanza leo wamelazimika kutembea kwa miguu, kufuatia madereva wa daladala na taksi kufunga barabara kwa zaidi ya saa tano ili kushinikiza uongozi wa jiji la Mwanza kuwaondoa wafanyabiashara ndogondogo maarufu kama machinga waliovamia eneo la stendi ya Tanganyika na kujigawia maeneo ya kufanyia biashara kinyemela.
Barabara zote za kuingia katikati ya jiji la Mwanza zilifungwa toka alfajiri baada ya madereva wa hiace na taksi kupaki magari yao katikakati ya barabara na kuyazima hali ambayo imesababisha usumbufu mkubwa kwa watumiaji wengine wa barabara, huku baadhi ya askari polisi wenye mbwa wakifanya doria kwa miguu na wengine kwa kutumia defender ili kukabiliana na vurugu ambazo zingeweza kujitokeza.
 
Baadhi ya wakazi wa jiji la Mwanza wamekerwa na kitendo hicho cha kufunga barabara na kusababisha kutembea kwa miguu huku wakiwa na mizigo, na kushauri kufanyika kwa mazungumzo ili kufikia muafaka kuhusu eneo hilo la stendi ya mabasi ya Tanganyika ambalo kabla ya machinga kulivamia na kujigawia maeneo ya kufanyia biashara zao lilikuwa likitumika kwa ajili ya maegesho ya magari ya mizgo aina ya canter na bodaboda.
 
Kufuati hali hiyo, mkurugenzi wa jiji la Mwanza Halifa Hassan Hida amewaagiza machinga waliovamia eneo la stendi ya Tanganyika pamoja na stendi ya daladala za Mwaloni- Kirumba, kupisha eneo hilo kwa muda hadi pale watakapotangaziwa rasmi.





No comments:

Post a Comment

Popular Posts