Thursday, January 22, 2015

MKUU WA MKOA WA NJOMBE AONYA VIONGOZI KUHUSU LUMBESA

 Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Rehema Nchimbi amewataka viongozi mkoani hapa na Iringa kuacha tabia ya kudai nyongeza wanaponunua mazao ya wakulima kwa sababu hiyo ni lumbesa.
Nchimbi alisema hayo jana katika mkutano wa wadau kutoka sekta ya umma na binafsi wa utekelezaji wa Sheria ya Mizani na Vipimo ya mwaka 1982.
“Nawaomba viongozi mbadilike kitabia, tuko hapa kuipiga vita lumbesa kwa sababu ni uvunjani wa sheria pia inatuharibia miundombinu ya barabara vijijini kutokana na uzito kuzidi. Lakini madhara yake mengine ni kumnyonya mkulima,” alisema Nchimbi.
Aliwataka wakulima na wafanyabiashara kuzinduka dhidi ya vipimo batili kwa kuunda kikosi kazi kitakachopambana na hali hiyo.
“Wanunuzi nao wana tabia ya kuomba kila kitu iwe sukari, chumvi na wakati mwingine hata nyama kwa sababu hawataki kutumia vipimo halali,” alisema Nchimbi.
Katibu Mtendaji Chama cha Wafanyabiashara wenye Viwanda na Kilimo (TCCIA) Mkoa wa Iringa, James Sizya alisema wameunda kikosi kazi kwa ajili ya kutekeleza sheria hiyo.
Alisema kikosi hicho kinajumuisha maofisa kilimo, biashara, polisi na wakulima.
Sizya alisema vita hiyo inatakiwa kuamshwa kwa kutoa elimu ili kufanikiwa.
Mwenyekiti wa TCCIA Mkoa wa Iringa, Lucas Mwakabungu alisema: “Muswada wa marekebisho ya sheria hiyo ulioandaliwa mwaka 2013 unapendekeza adhabu iongezwe kwa kuwa faini ya sasa ni Sh100,000 ni ndogo,” alisema Mwakabungu.

No comments:

Post a Comment

Popular Posts