Saturday, January 24, 2015

Natamani kuonana na Rais Kikwete nimweleze ukweli

 

Baada ya kufanikisha lengo la kuonana na familia zaidi ya 30 za Watanzania waliofungwa katika magereza mbalimbali Hong Kong, Padri wa Kanisa Katoliki, John Wootherspoon aliyeleta ujumbe wa watu hao amesema anatamani kuonana na Rais Jakaya Kikwete ili amweleze hali ya biashara ya dawa za kulevya na manung’uniko ya wafungwa hao.
 
“Nilichoona ni kuwa Tanzania imetawaliwa na rushwa, vijana wengi wanaingia katika dawa za kulevya kwa sababu ya umaskini. Umaskini wenyewe naona kuwa kiini chake ni rushwa. Natamani nizungumze naye iwapo atakubali,” alisema Padri Wootherspoon.
 
Akizungumza na gazeti la Mwananchi, Wootherspoon, raia wa Australia na padri wa parokia ya Notre Dame, Shing Tak Street, Hong Kong, Kowloon, anasema anatamani azungumze na Rais Kikwete ili amweleze hali halisi ya biashara ya dawa za kulevya kwani kukutana kwake na wafungwa wa Kitanzania mjini Hong Kong kumempa fursa ya kujua mengi.
 
Katika ziara yake ya hapa nchini ya kutembelea familia za wafungwa hao wa dawa za kulevya kwenye magereza ya Hong Kong, Macau na Guang Zhou, Padri Wootherspoon pia alionana na kamishna wa Kitengo cha Kupambana na Dawa za Kulevya, Godfrey Nzowa.
 
Kadhalika Wootherspoon alisema kati ya mengi aliyonayo, anatamani kumwambia Rais afanye kila liwezekanalo ili kuhakikisha Watanzania hao wanarudishwa nchini kama Nigeria ilivyofanikiwa.
 
“Hata kitengo cha Haki za Binadamu cha Umoja wa Mataifa kinaeleza wazi kuwa, mfungwa ana haki ya kuhukumiwa katika nchi yake. Lakini nashangaa kuona kwa nini suala hili limekuwa gumu kufanikiwa hapa,” alisema.
 
Akihutubia taifa katika sherehe za kilele cha mbio za Mwenge mwaka jana mkoani Tabora, Rais Kikwete alisema serikali imefanya jitihada mbalimbali za kukabiliana na uingizwaji wa dawa hizo, hali aliyosema imesaidia kuwakata wasafirishaji wanaotumia njia mbalimbali kusafirisha dawa hizo.


Wootherspoon alisema anaamini kuwa Rais Kikwete ni mkarimu, mwelewa na amejaribu kulivalia njuga suala hili la dawa za kulevya, lakini imekuwa vigumu kwake kufanikisha kutokana na mazingira.
 
“Nia yangu kubwa ni kuwafanya vijana wasiende tena nchi za mashariki ya mbali. Huko kuna hatari ya kunyongwa, si kuzuri. Wasikubali pia kutumiwa na hawa wafanyabiashara wakubwa wa dawa za kulevya. Ombi langu ni kutaka waache kufanya biashara hiyo,” alisisitiza.
 
Tatizo bado kubwa
Wafungwa hao ambao wengi wanatumikia kifungo cha maisha na wengine kati ya miaka 20 hadi 25, wanalalamika kuwa matajiri wanaowatuma hawachukuliwi hatua za kisheria, licha ya wao kuwataja kwa majina na kuweka wazi ushahidi kwa viongozi wa Serikali wanaowatembelea magerezani, China.
 
Hata hivyo, Nzowa alisema kuwa tayari magwiji wa dawa za kulevya waliokuwa wanaipa serikali wakati mgumu, wameshatiwa nguvuni na kilichobaki ni hukumu tu.
 
Bila ya kuwataja vigogo hao, Kamishna Nzowa anasema kesi zao tayari zimeshafikishwa mahakamani na kuwa wengi walishikwa na vithibiti, hali inayofanya kesi zao kuwa nyepesi kukamilika.
 
"Tulifanya kila tuwezalo tukawamata magwiji wenyewe, ambao wanawatumia vijana kubeba dawa hizo. Kwa sasa asilimia kubwa tayari tumewakamata lakini bado kazi haijamalizika kama tunavyodhani. Huu mtandao ni mkubwa,” alisema.











No comments:

Post a Comment

Popular Posts